Wednesday, February 13, 2013

JK awatosa CC wawania urais 2015

MWENYEKITI wa CCM, Rais Jakaya Kikwete ameamua kuwatosa vinara wanaotajwa kutaka kuwania urais kupitia chama hicho kutoingia kwenye Kamati Kuu (CC).
Dalili za kuwatosa vinara wanaotajwa kuwania urais 2015, ni kutokana na hatua yake ya juzi kuamua kutowapendekeza kuwa miongoni mwa majina ambayo yangepigiwa kura ili kuweza kuingia katika CC.

Wachambuzi wa masuala ya kisiasa ndani na nje ya CCM wanaona hatua ya Kikwete kutopendekeza majina ya wanasiasa vigogo wanaotaka urais 2015 kupitia chama hicho katika orodha ya watu 42 ili kuwania nafasi 14 za CC kama mkakati maalumu wa kuwaweka kando.

Hata hivyo, mkakati huu wa Kikwete ulikuwa hatua muhimu kwake kama kiongozi wa chama baada ya kukwama kuzuia makundi kung’ara katika chaguzi zilizopita ambapo wafuasi wa Edward Lowassa waliibuka kidedea kuanzia katika NEC, mikoani na Jumuiya za chama hicho.
Ndiyo maana baada ya kumalizika Uchaguzi wa wajumbe wa NEC, Kikwete alisita kuunda CC kwa maelezo kwamba waliochaguliwa walikuwa wageni na alikuwa hawafamu vizuri. Hatua hii ya Kikwete ilitafsiriwa kama mkakati wa kuzima nguvu ya mojawapo ya kambi.
Hata hivyo, kuna mtazamo tofauti kwamba hatua ya Kikwete kutopendekeza majina makubwa na yenye nguvu ndani ya CCM kuwania ujumbe wa Kamati Kuu inaweza ikawa ni njia ya kuwafanya wajumbe wa CC kuwa na kazi moja tu ambayo ni kuchuja majina ya wagombea badala ya wao pia kuwa washiriki.

Kutoswa kwa vigogo
Katika hali iliyozua gumzo, majina ya wanasiasa vigogo Edward Lowassa, Benard Membe na Samuel Sitta ha yakuwamo katika orodha ya Rais Kikwete aliyowasilisha mbele ya NEC ili kupata wajumbe wa CC, ambacho ni chombo muhimu cha uamuzi ndani ya chama hicho.

Lowassa, Membe na Sitta ndiyo wanaelezewa kuwa na makundi makubwa yana yowaunga mkono kiasi cha kutishia uhai wa chama hicho katika chaguzi zijazo.
Makundi ya watu hao yamekuwa hasimu kiasi cha wakati fulani, Kikwete kulazimika kuunda kamati ya watu watatu chini ya Rais Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi, Makamu Mwenyekiti wa zamani wa chama hicho, Pius Msekwa na Abdulrahman Kinana, ambaye ni Katibu Mkuu wa chama hicho kwa sasa ili kusuluhisha mgogoro huo.

Hata hivyo, kansa ya mgogoro imeendelea na kujipambanua waziwazi na hasa wakati wa Uchaguzi Mkuu wa chama hicho mwaka jana wakati makundi hayo yalipopambana kujaza wafuasi wao kwenye NEC kwa lengo la kujipanga kwa ajili ya uchagzui wa 2015.

Wafuatiliaji wa siasa za CCM wanaamini kukosekana kwa Lowassa, Membe na Sitta bila shaka ni pigo kwa mbio za wanasiasa hao kutaka kuingia Ikulu mwaka 2015.
Kwani kama watapenya kwenye kinyang’anyiro cha kuwania urais kupitia CCM mwaka 2015 watakuwa wamefuata nyayo za Benjamin Mkapa ambaye aliteuliwa kugombea urais akiwa si mjumbe wa CC.

Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi na Kikwete walikuwa wajumbe wa CC kabla ya uteuzi wao kugombea urais.

Maoni ya watu mbalimbali
Baada ya CCM kuhitimisha safu yake ya uongozi kwa Halmashauri Kuu ya chama hicho (NEC) kuchagua wajumbe CC huku kikiwatosa wanaotajwa kutaka kuwania urais 2015, baadhi ya wasomi wamesema kitendo hicho kinaonyesha kuwa chama hicho tawala kimedhamiria kujiimarisha.

Wakitoa maoni kwa nyakati tofauti wasomi hao walisema hali ingekuwa mbaya ndani ya chama hicho kama baadhi ya watu hao wangechaguliwa kuwa wajumbe wa CC.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Profesa Gaudence Mpangala alisema kutopendekezwa kwa Lowassa, Membe na Sitta kulitarajiwa kwa kuwa viongozi wengi wa chama hicho walikuwa hawapendi jinsi baadhi ya wanachama wa CCM wanavyoonyesha wazi dhamira yao ya kuutaka urais.

“Inawezekana uamuzi wa CC ukawa na malengo mapana likiwamo hili, inawezekana chama kiliona kikiyapitisha majina hayo kitaleta mtafaruku na maneno ya hapa na pale,” alisema Profesa Mpangala.

Mpangala alisema Rais kama Mwenyekiti wa CCM lazima awe na mipango yake ya kuhakikisha kuwa anatengeneza mtu wa kuchukua nafasi yake na ambaye wanaelewana.
Naye Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Bashiru Ally alisema atakayependekezwa kugombea urais ndani ya CCM, siyo lazima awe mjumbe wa Kamati Kuu au Halmashauri Kuu.
“Ujumbe tu hautoshi, mtu anaweza asiwe mjumbe wa NEC wala Kamati Kuu, lakini akawa na ushawishi mkubwa ndani ya vyombo hivyo pamoja na Mkutano Mkuu wa chama hicho,” alisema Bashiru.

“Wapo wagombea urais mwaka 2005 walienguliwa licha ya kuwa na majina makubwa, nadhani sifa ya mgombea ndiyo kitu cha kwanza” alisema Bashiru akitolea mfano wa John Malecela, ambaye alikuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM wakati huo.
Kwa upande wake, mwanasiasa kijana David Kafulila anaona uamuzi wa Kikwete kutowapendekeza wanaotajwa kuwania urais ndani ya chama hicho kama mkakati wa kufanya wajumbe wa CC wawe na kazi moja tu ambayo ni kuchuja wagombea.

“Nadhani Kikwete anaweza akawa na mkakati wa kufanya wajumbe wa CC wasiwe wachezaji wakati wa kuwania kupeperusha bendera ya CCM 2015, lakini inaweza ikawa ni mkakati wa kuwapunguzia nguvu za kutimiza malengo yao,” alisema Kafulila ambaye ni mbunge wa Kigoma Kusini kwa tiketi ya NCCR-Mageuzi.

Waliochaguliwa kuingia kwenye Kamati Kuu kutokea Tanzania Bara ni pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo Mijini, Profesa Anna Tibaijuka na Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Rais, Steven Wassira.
Wengine ni Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Bunge), William Lukuvi, Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Dodoma, Alhaji Adam Kimbisa, Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Silaa na Mbunge wa Viti Maalumu, Pindi Chana.

Kutoka Tanzania Visiwani mbali na Dk Salim, wengine ni Waziri wa Ulinzi, Shamsi Vuai Nahodha, Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hussein Mwinyi.

Pia wamo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Suluhu Hassan, Naibu Waziri wa zamani wa Mawasiliano na Uchukuzi, Dk Maua Abeid Daftari pamoja na Khadija Aboud

Wajumbe wa NEC mtegoni
Rais Kikwete pia aliwataka wajumbe wa CC na wale wa NEC waheshimu kazi za wabunge kwenye majimbo yao ili wawape nafasi ya kutekeleza walichokiahidi.
Akitambulisha wajumbe wapya wa CC, alidai kitendo cha baadhi ya wajumbe hao kupita katika majimbo na kuanza kufanya kazi za kuwakosoa wabunge hakifai kuvumiliwa na mara nyingi kinakuwa ni chanzo cha migogoro na kuwafanya baadhi ya watu kushindwa kutekeleza Ilani ya CCM.

“Si kwamba msiende hapana, nendeni mkazungumzie utekelezaji wa Ilani, lakini habari za kuwavuruga wabunge iwe ni marufuku hadi uchaguzi utakapifika,” aliongeza Kikwete na kumtaka Makamu Mwenyek iti wa CCM kwa upande wa Tanzania Bara, Phillip Mangula kuwachukulia hatua kali wahusika.

Kiongozi Bavicha avaa gwanda la kijani
Aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Juliana Shonza jana alimtumia salamu mbunge wa Ubungo, John Mnyika kuwa asahau ndoto za kulipata jimbo hilo tena.
Mbali na hilo, aliwataka Watanzania kumpelekea ujumbe kwa wabunge wa Chadema wa Mkoa wa Mbeya kuwa wakae mkao wa kula kwani hayuko tayari kuona mkoa aliozaliwa yeye ukiongozwa na Chadema.

Shonza alitoa kauli hiyo jana katika Viwanja vya CCM Mjini hapa ikiwa ni muda mfupi tangu akabidhi kadi ya Chadema kwa Kikwete na kujiunga rasmi na CCM.
Mbali na Shonza mwingine aliyejiunga jana alikuwa ni Mtera Mwampamba ambaye mwaka 2010 alikuwa ni mgombea ubunge wa Jimbo la Mbozi Mashariki.

Jimbo hilo kwa sasa linaongozwa na Mwenyekiti CCM Mkoa wa Mbeya, Godfrey Zambi.
Huku akishangilia na umati mkubwa wakazi wa Mji wa Dodoma waliofurika katika viwanja hivyo, Shonza alianza kwa kumwomba radhi Rais Kikwete kuwa alikuwa akitumika vibaya kwa kumtukana majukwaani, lakini akasema anajutia kosa lake na kwamba kwa sasa yuko tayari kumsaidia Rais.
“Nimekosa Rais, naomba unisamehe mimi na vijana wenzangu, lakini nikiwa na muda mzuri nitawaeleza Watanzania yaliyoko Chadema na kamwe sijutii uamuzi huo wa kujiunga na CCM,” alisema

Nape adai wengine wanafuata
Kwa upande wake, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema kuwa kuwapokea vijana hao ni mwanzo, lakini Watanzania wategemee kupokea watu wengi zaidi.
Nape alisema hivi sasa wameanza na kikosi kipya cha ushindi ambacho walitangaza kuwa ni kikosi cha ushindi mwaka 2015 na akasema walioko nyuma ya Shonza na Mwampamba ni wengi zaidi.

“Nawakaribisha wananchi siku ya Jumamosi ijayo jijini Dar es Salaam, lazima tutatikisa kwa kishindo na kuwapokea vijana wengi, tumeamua na sasa kazi ni moja lazima waishe huko,” alijinasibu Nape.

Chadema wanena
Akizungumzia kitendo hicho, Mwenyekiti wa Bavicha, John Heche alisema usalama wa Chadema uko makini zaidi ya Usalama wa Taifa, kwamba haiwezekani wanaCCM kufanya shughuli za chama hicho akiwa Chadema.

“Huku alikoenda ndio kunamfaa, Chadema na hasa Bavicha tulijua kuwa (Shonza) alikuwa CCM tangu siku nyingi na alichokifanya sasa ni kuthibitisha tu,” alisema Heche ambaye aliingia katika mgogoro wa muda mrefu na Shonza kabla ya kutimuliwa.
Kwa upande wake, Mnyika alisita kuitolea ufafanuzi kauli ya Shonza kwamba anataka kuwania ubunge katika jimbo hilo.

“Ninachoweza kusema ni kwamba (Shonza) anachotakiwa kufanya ni kupigania apitishwe na chama chake katika kura za maoni ili awanie ubunge” alisema Mnyika.

Mauaji ya Geita
Naye Rais Kikwete alilaani mauaji yaliyotokea Geita na kusababisha kifo cha mchungaji wa Kanisa la Assemblies Of God, Mathayo Kachila (45) na wengine 15 kujeruhiwa katika machafuko hayo.

Alisema tangu historia ya Tanzania ambayo ni zaidi ya miaka 50 hapajawahi kutokea mapigano ya udini, lakini sasa yameonekana kwa mara ya kwanza jambo linalohitaji kila mmoja kulilaani.

Habari kutoka  Mwananchi.co

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...