WAKATI kukiwa na taarifa kwamba maofisa wa Shirika la Upelelezi 
la Marekani (FBI) wametua nchini kwa ajili ya kufanya upelelezi wa 
mauaji ya Padri Evarist Mushi, Jeshi la Polisi limetangaza dau la Sh10 
milioni kwa atakayefichua aliyemuua padri huyo.
Padri Mushi aliuawa kwa kupigwa risasi Jumapili 
iliyopita wakati akienda kuongoza ibada katika Kanisa la Mtakatifu 
Teresia lililopo Beit el Ras nje kidogo ya mji wa Zanzibar, ambapo 
inadaiwa kuwa waliomuua walikuwa wamepanda pikipiki aina ya Vespa na 
walimfyatulia padri huyo risasi tatu akiwa ndani la gari yake.
Wakati polisi wakitangaza dau hilo, Sheikh Ali 
Khamis Ali (65) mkazi wa Kitope Kaskazini Unguja, aliuawa jana kwa 
kukatwa mapanga mjini Zanzibar, baada ya wezi kuvamia shambani kwake.
Habari za kuaminika zilizopatikana juzi zinaeleza 
kuwa maofisa hao wa FBI, wako nchini na tayari na wamekutana na baadhi 
ya viongozi wa Serikali kwa ajili ya kuanza kazi hiyo.
Chanzo chetu cha habari kimeeleza kuwa maofisa hao
 walikutana na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi kwa
 ajili ya kuangalia ni namna gani watafanya shughuli zao katika 
upelelezi huo.
Pamoja na ushiriki FBI, taarifa zinaeleza kuwa 
maofisa wa Serikali ya Tanzania wamezungumza na taasisi za upelelezi za 
nchi tano, ili kuongeza nguvu katika upelelezi huo.
Taasisi nyingine inayotajwa kuwa huenda ikashiriki
 katika uchunguzi huo ni Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai ya 
Uingereza (Scotland Yard).
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Pereira Ame Silima
 alilithibitishia gazeti hili kwamba Serikali imeanza kufanya mazungumzo
 na mashirika mbalimbali ya upelelezi duniani kwa ajili ya kushirikiana 
nayo kuchunguza mauaji ya Padri Mushi, lakini akasema kuwa ni mapema mno
 kuyataja.
“Tumefuata maagizo aliyotoa Rais Kikwete kwamba 
tushirikishe mataifa mbalimbali kuchunguza mauaji yaliyotokea Zanzibar, 
siwezi kutaja kwa majina, ila tayari tumeanza kuzungumza na nchi 
mbalimbali,” alisema Silima.
Akizungumza mjini Zanzibar jana, Kamishna wa 
Polisi visiwani humo, Mussa Ali Mussa alisema kuwa hadi sasa hakuna mtu 
aliyefikishwa mahakamani kuhusiana na tukio hilo la mauaji.
“Hakuna aliyefikishwa mahakamani, lakini wapo watu
 ambao wamekamatwa wakihusishwa na tukio hili na tunaendelea kuwahoji, 
wengine tunawaachia,” alisema na kuongeza:
“Tumeahidi kutoa Sh10 milioni kwa mtu yeyote, atakayetoa taarifa za mauaji ya Padri Mushi, hii itakuwa kama zawadi tu.”
Habari zilizopatikana zinaeleza kuwa maofisa wa FBI wamekutana 
na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Said Mwema kuzungumzia suala hilo la 
mauaji ya Padri Mushi.
Tukio hili la kuuawa kwa Padri Mushi linahusishwa 
na matukio kadhaa ya vurugu zilizoambatana na uchomaji moto makanisa na 
mali mbalimbali hivi karibuni.
Moja ya matukio hayo ni lile la Jumatano ya 
Desemba 25 mwaka jana ambapo Padri wa Kanisa Katoliki lililopo Mpendae 
visiwani Zanzibar, Ambrose Mkenda, alijeruhiwa kwa risasi na watu 
wasiojulikana nje ya nyumba yake, saa 12 jioni wakati akitoka kanisani.
Padri huyo alipatiwa matibabu katika Hospitali Kuu
 ya Mnazi Mmoja na baadaye alihamishiwa katika Hospitali ya Taifa 
Muhimbili kwa matibabu zaidi.
Wakati huo huo, Sheikh Mussa Ali Mussa ambaye alikuwa kiongozi wa Misikiti ya Kitope na Mwakaje ameuawa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kaskazini Unguja, Ahmada
 Khamis alisema kuwa kiongozi huyo, aliuawa kutokana na kipigo 
alichokipata kutoka kwa wezi waliovamia shamba lake.
Kuuawa kwa Sheikh huyo kumezua hofu kwa wakazi wa 
Zanzibar wakidhani ni kitendo cha kulipiza kisasi, lakini Polisi 
imetuliza hali hiyo kwa kusema kwamba aliuawa na wezi waliokuwa wakiiba 
shambani kwake.
Alisema kwamba baada ya kuwafuma wezi hao wakiiba 
shambani kwake walimshambulia kwa mapanga na kupoteza uhai wake na 
kwamba hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo.
Habari imeandikwa kwenye mwananchi.co.tz


 
 
























 
 
 
 
