Habari Leo, SHINYANGA
Mkazi
 wa Ndembezi mjini Shinyanga amepigwa na mumewe hadi kuzirai na 
kukimbizwa hospitalini kwa matibabu baada ya kutoa ushirikiano kwa 
karani wa Sensa ya Watu na Makazi.
Kamanda
 wa Polisi wa Mkoa huo, Evarist Mangala, alisema jana kuwa mwanamke 
huyo, Esther Zablon (40) alipigwa juzi saa mbili asubuhi baada ya 
mumewe, Ismail Yahya kupata taarifa kuwa karani wa sensa alifika 
nyumbani kwao na mkewe kukubali kuhesabiwa na kutoa takwimu za familia 
yao.
Akisimulia,
 Kamanda Mangala alisema karani huyo alipokwenda nyumbani hapo, mume 
hakuwapo na kama mkuu wa kaya, Esther akazungumza na kutoa taarifa.
Alisema
 baada ya mume kurudi nyumbani na kugundua kuwa mkewe alikubali 
kuhesabiwa, alimshambulia kwa ngumi na mateke na kusababisha mke huyo 
kupoteza fahamu.
Kutokana na kipigo hicho, kwa mujibu wa Kamanda Mangala, Esther alikimbizwa katika Hospitali ya Mkoa kwa uchunguzi na matibabu.
"Wakati
 mwanamke huyo akichukua fomu namba tatu ya Polisi (PF3) kituoni kabla 
ya kufikishwa hospitalini, huku akilia kuwa sababu ya kipigo ni yeye 
kukubali kuhesabiwa, jambo ambalo ni kinyume na msimamo wa dini ya 
mumewe (Uislamu)," alisema Kamanda Mangala.
Hata hivyo, Kamanda alisema Esther alitoroka wodini kwa kuhofia mumewe kukamatwa na hatimaye kufungwa.
Kamanda Mangala alisema Polisi wanaendelea kumtafuta Yahya na akipatikana atafikishwa mahakamani kujibu mashitaka yanayomkabili.


 
 










 
 
 
 
