na Tamali Vullu, Dodoma
SERIKALI imesema katika mwaka huu wa fedha, itatengeneza ajira 800,000 katika fani mbalimbali nchini.
Kauli
 hiyo ya serikali ilitolewa bungeni jana na Waziri wa Kazi na Ajira, 
Gaudensia Kabaka, alipokuwa akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi
 kwa wizara yake kwa mwaka 2012/2013.
Alisema
 fursa za ajira hizo mpya zitapatikana kupitia miradi ya maendeleo chini
 ya mpango wa taifa wa miaka mitano unaotekelezwa na wizara na taasisi 
mbalimbali ((FYDP I).
“Takwimu
 hizi ni mbali na ajira za watumishi 56,678 watakaoajiriwa na serikali 
kama ilivyobainishwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya 
Utumishi wa Umma, ” alisema.
Waziri Kabaka alisema ajira hizo zitapatikana katika sekta za kilimo, ujenzi, mawasiliano na viwanda.
“Ajira
 zitakazozalishwa katika Kilimo ni 169,189, ujenzi wa miundombinu ya 
barabara 646,615, mawasiliano 27,600 na katika sekta ya viwanda na 
biashara zitazalishwa ajira 5,000,” alisema.
Alibainisha kuwa katika mpango huo wa kuongeza ajira, halmashauri za mikoa ya Dar es Salaam na Pwani zitazalisha ajira 6,885.
Alieleza kuwa katika mwaka wa fedha ulioisha, jumla ya ajira 250,678 zilipatikana kutokana na miradi ya maendeleo.
Alisema
 ajira zilizopatikana katika miradi mbalimbali ikiwemo Tasaf (34,516), 
ujenzi wa barabara (42,107) na ujenzi wa majengo ya serikali (17,685).
Miradi
 mingine kituo cha taifa cha uwekezaji (TIC) ajira 82,834, mamlaka ya 
ukanda wa kiuchumi (EPZA) 15,100 na serikali ilitengeneza ajira 38,289.
Source: Tanzania Daima

 
 









 
 
 
 
