na Betty Kangonga
KUTEKWA,
 kupigwa na kuteswa kwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Chama cha Madaktari 
nchini, Dk. Steven Ulimboka na hatimaye kufungiwa kwa Gazeti la 
MwanaHalisi kwa muda usiojulikana, kumeleta kizaazaa katika kampuni ya 
simu za mkononi ya Tigo, Tanzania Daima Jumatano limebaini.
Habari
 kutoka ndani ya kampuni hiyo ya simu yenye mtandao mpana nchini, 
zinasema kuwa zaidi ya wafanyakazi 30 wamefukuzwa kazi na wengine wako 
kwenye uchunguzi wakituhumiwa kuvujisha mawasilino ya siri ya simu za 
wateja kwa Gazeti la MwanaHalisi.
Kwa
 mujibu wa habari hizo, taarifa za mawasiliano za simu zinazodaiwa 
kuvujishwa na wafanyakazi hao, zilikuwa kati ya Dk. Ulimboka, Afisa 
Usalama wa Ikulu na watu aliowasiliana nao kabla ya kutekwa.
Rais
 Jakaya Kikwete amepata kuliambia taifa mara mbili kwa njia ya 
televisheni, mwishoni mwa Juni na alipozungumza na wahariri wa vyombo 
vya habari wiki iliyopita, kwamba serikali yake haihusiki kuteka, kutesa
 na kumtupa daktari huyo porini.
Naye
 Waziri Mkuu Mizengo Pinda amepata kuliambia Bunge kuwa, serikali yake 
haihusiki na utekaji, utesaji na kuhoji, “...serikali imteke ili iweje?”
Hivi
 karibuni serikali ililifungia Gazeti la MwanaHalisi baada ya kuandika 
habari iliyomtaja ofisa mmoja wa Idara ya Usalama wa Taifa Ikulu (TISS),
 kuwa ndiye aliyetekeleza mpango wa kumteka, kumpiga na kumtesa hadi 
kumjeruhi Dk. Ulimboka, ambaye kwa sasa anaendelea na matibabu kwenye 
hospitali moja nchini Afrika Kusini.
Kwa
 mujibu wa habari hiyo ambayo serikali inadai kuwa ni ya uchochezi, 
MwanaHalisi ilianika namba ya simu ya ofisa huyo pamoja na watu wengine 
wanaodaiwa kuhusika katika tukio hilo linaloendelea kuchunguzwa na 
kamati maalumu iliyoundwa na Ofisi ya Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai 
(DCI).
Vyanzo
 vya habari kutoka kwa baadhi ya wafanyakazi waliokumbwa na sekeseke 
hilo, zinasema kuwa waliofukuzwa wengi ni wafanyakazi wa kitengo cha IT 
ambao wanadaiwa kuhusika kutoa taarifa za siri ya mawasilino kati ya Dk.
 Ulimboka na watu wanaoaminika kuwa ni wabaya wake.
Mmoja
 wa wafanyakazi kutoka Kampuni ya Tigo, aliliambia gazeti hili kuwa 
mbali na kutuhumiwa kutoa siri kwa Gazeti la MwanaHalisi, wafanyakazi 
wengine wametimuliwa kwa madai ya kufanya udanganyifu kwenye huduma za 
Tigo Pesa na kujipatia fedha.
“Kweli
 watu wengi wamefukuzwa wakituhumiwa kutoa siri kwa Gazeti la 
MwanaHalisi, lakini wengine walikuwa wakishirikiana na mawakala wa Tigo 
Pesa kuiibia kampuni.
“Kwa
 mfano mfanyakazi alikuwa anakubaliana na wakala kumwingizia kiasi kama 
cha sh milioni moja, lakini anaweza kuingiza hadi sh milioni 1.5 na kati
 ya hizo sh 500,000 ni mali yake,” alisema mfanyakazi huyo.
Akizungumzia
 na Tanzania Daima Jumatano, Mhariri Mkuu wa Gazeti la MwanaHalisi, 
Jabir Idrissa alishangazwa na taarifa za Tigo kuwafukuza wafanyakazi 
wake kwa sababu ya habari iliyochapishwa na gazeti lake.
“Chanzo
 chetu cha habari hakikutoka kwa wafanyakazi wa Tigo. Kama wamefukuzwa 
kwa sababu ya MwanaHalisi, wamewaonea bure. Kama Tigo ndio waliotupa 
taarifa na zile za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), zilitoka wapi?” 
alihoji Jabir na kusisitiza wafanyakazi hao wameonewa bure.
Ofisa
 Uhusiano wa Tigo, Edward Shila, alipohojiwa kuzungumzia tukio hilo, 
hakukubali wala kukataa madai hayo na kumtaka mwandishi kumtumia maswali
 kupitia e-mail yake ili aweze kuyatolea majibu kiofisi.
“Kama
 una maswali naomba uniandikie kupitia e-mail yangu ambayo nakutumia 
sasa hivi…maana siko tayari kutoa kauli yoyote isiyokuwa ya kiofisi,” 
alisema.
Naye
 Omary Matulla ambaye amejitambulisha kuwa ni ofisa wa kitengo cha 
kumbukumbu katika kampuni hiyo, alikanusha kuwapo kwa taarifa za 
kufukuzwa wafanyakazi wa kampuni hiyo.
Alisema
 kuwa kila mfanyakazi ana mipaka ya kufanya kazi katika kampuni hiyo, na
 pia ni wajibu wa kila mtumishi kutunza siri kubwa.
“MwanaHalisi
 ana mbinu zake za kupata habari wala haiwezekani kupata habari kupitia 
kampuni yetu na hata hivyo jambo hilo si rahisi hata kidogo kutokea,” 
alikanusha Omary.
Dk.
 Ulimboka alitekwa usiku wa Juni 26, kusukumizwa kwenye gari, kupigwa, 
kufungwa mikono na miguu, kunyofolewa kucha na kutolewa meno na hatimaye
 kutupwa katika msitu wa Mabwepande nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.
Tangu
 kutokea kwa tukio la kutekwa kwa Dk. Ulimboka, Chama cha Demokrasia na 
Maendeleo (CHADEMA) na wanaharakati wa kutetea haki za binadamu, 
wamekuwa wakiinyoshea kidole serikali kwamba ndiyo iliyohusika.
Kamanda
 wa Kanda Maalumu ya Polisi mkoani Dar es Salaam, Suleiman Kova, hivi 
karibuni alitangaza kumfikisha mahakamani mtu mmoja aliyedai kukiri 
kuhusika na utekaji wa Dk. Ulimboka.
Kova
 aliwaambia waandishi wa habari kuwa, polisi wamekamata mtu aitwaye 
Joshua Malundi kutoka Kenya ambaye amekiri kumteka na kumtesa Dk. 
Ulimboka.
Alidai kuwa mtuhumiwa alikwenda kutubu katika Kanisa la Ufufuo na Uzima, Kawe, Dar es Salaam.
Lakini
 hata hivyo, mchungaji wa kanisa hilo, Josephat Gwajima alikana kauli ya
 Kova juu ya mtuhumiwa huyo, akisema hajakwenda kutubu kwao.
Source: Tanzania Daima

 
 









 
 
 
 
