Wednesday, August 10, 2011

Wauza mafuta wabanwa, watakiwa kujieleza


MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), imetoa amri kwa kampuni nne kubwa zinazosambaza mafuta kurejesha huduma hiyo mara moja huku ikizitaka kujieleza, kwa nini zisichukuliwe hatua za kinidhamu kwa kushindwa kutimiza wajibu wao kwa mujibu wa leseni zao za biashara.

Kampuni hizo ni pamoja na BP ambayo Serikali inamiliki nusu ya hisa pamoja na Engen, Oil Com na Camel. Mbali ya maagizo hayo mawili, Ewura pia imezitaka kampuni hizo kuhakikisha kwamba zinaendelea kutoa huduma hiyo bila kubughudhi mfumo wa usambazaji mafuta nchini.

Aidha, Ewura pia imetoa leseni kwa Shirika la Taifa la Maendeleo ya Petroli (TPDC) kuingiza mafuta kuanzia jana ikisema ombi lake la kupatiwa leseni ya kuuza ndani ya nchi litashughulikiwa baada ya kubainisha miundombinu yake.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Haruna Masebu alisema kisheria, amri hiyo (Compliance Order) ni sawa na agizo la Mahakama Kuu na kwamba wahusika hawana budi kutii. Mbali na kampuni hizo, Masebu alisema pia kwamba kampuni nyingine ndogo za mafuta zinachunguzwa na zitakazothibitika kuhusika katika mgomo wa kutoa huduma hiyo muhimu ya nishati, zitachukuliwa hatua.

Agizo la Ewura limekuja sambamba na hatua ya Bunge kusitisha shughuli yake kawaida jana ambayo ilikuwa ni mjadala wa hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara na kujadili mgomo wa wafanyabiashara ya mafuta ambao mpaka jana, walikuwa wamesitisha uuzaji wa bidhaa hiyo katika vituo mbalimbali nchini na kusababisha kusimama kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii. Ombi la kujadili suala hilo liliwasilishwa bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya bunge ya Nishati na Madini, January Makamba.

Baada ya mjadala uliochukua sehemu kubwa ya shughuli zake za jana, Bunge liliazimia kwa kauli moja kwamba Serikali ihakikishe amri hiyo ya Ewura kama ilivyowasilishwa kwake na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja inatekelezwa.

Akihitimisha hoja yake, Makamba alitoa hoja kwamba sheria ifuate mkondo wake na kuitaka Serikali kuchukua hatua kwa kampuni zitakayokaidi agizo hilo mara baada ya muda uliotolewa kumalizika. Pia alisema: “Kwa sababu tatizo hili ni la nchi nzima na watakaoanza kunufaika ni wakazi wa Dar es Salaam, Serikali ihakikishe kuwa na mikoani mafuta yanapatikana kama kawaida.”
Wananchi wakiwa katika foleni wakisubiri kununua mafuta katika moja ya vituo vinavyouza nishati hiyo jijini Dar es Salaam.(Picha na Evance Ng'ingo).

source--habarileo & mwananchi 

0 comments:

Post a Comment

CHANGIA MAWAZO YAKO HAPA

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...