Tuesday, June 25, 2013

‘Ambulance’ iliyombeba Mzee Madiba iliharibika

Gari hilo la kubebea wagonjwa liliharibika mitambo yake likiwa njiani ambapo lilikaa dakika 40

Afrika Kusini. Rais wa zamani wa Afrika Kusini Nelson Mandela maarufu kama Madiba imedaiwa alipata wakati mgumu wakati akielekea hospitalini baada ya gari la wagonjwa lililokuwa likimsafirisha wiki mbili zilizopita, kuharibika mitambo likiwa njiani kwenda hospitalini.
Taarifa za kuharibika kwa gari hilo zilitolewa juzi na msemaji wa rais wa Afrika Kusini Mac Maharaj, ambaye alidhibitisha kuwa gari hilo lilipata  matatizo na ililazimika  Rais huyo wa zamani kuhamishiwa katika gari nyingine.
Hata hivyo Maharaj, alisema tukio hilo halikuwa na tishio lolote kwa afya ya mzee  Mandela, kwa sababu aliongozana  na madaktari wa kutosha.
Dakika 40
Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Marekani CBS  lilisema kuwa vyanzo kadhaa vilidai kuwa Mandela alilazimika kukaa eneo hilo ambapo gari  hilo la wagonjwa liliharibika kwa muda wa dakika 40.

Shirika hilo la CBS lilisema kuwa wakati Mandela alipokuwa akihamishwa katika  gari nyingine viwango vya joto vilikuwa chini sana.
Mandela alilazwa hospitalini huku hali yake ikiwa mbaya kutokana na maambukizi ya mapafu ya mara kwa mara na tangu wakati huo alikuwa katika chumba cha wagonjwa mahututi.
Hii ni mara ya tatu kwa Mandela kulazwa hospitalini mwaka huu.
Mandela, aliye na umri wa miaka 94, alilazwa hospitalini mnamo Juni 8, baada ya kupata matatizo ya kupumua, ugonjwa ambao umekuwa ukimsumbua mara kwa mara.
Akiongea na Shirika la Habari la Enca, Mac Maharaj alisema kuwa ‘hakuna tatizo lililotokea’ kwani walikuwa makini, wakati wa tukio hilo.
Alipotakiwa kutoa maelezo kwamba ilikuwaje gari la kubebea wagonjwa  ilitumike ikiwa  na hitilafu za kimitambo  alisema  “Hili ni tukio la kawaida. Hakuna anayeweza kutarajia kuwa gari lililokuwa likienda vizuri lingeweza kukumbwa na hitilafu za kimitambo.”

Ini na figo
Taarifa za ndani zilisema kwamba  ini na figo za rais huyo wa zamani zilikuwa zikifanya kazi kwa asilimia 50. Kiongozi huyo vile vile alitarajiwa kufanyiwa upasuaji maalumu  kuziba kidonda kilichokuwa kikivunja damu.
Kwa mujibu wa mjukuu wa  Madiba, Ndaba Mandela alisema babu yake  alikuwa akiendelea vyema na alikuwa akitarajiwa kuwa atatoka hospitalini hivi karibuni.
 “Ni Mungu pekee anayeweza kumchukua…sisi kama familia tutazidi kushukuru na kusherekea maisha yake,”alisema  Ndaba Mandela.
Wakati huohuo mmoja wa wanaharakati wa kupinga ubaguzi wa rangi nchini Afrika Kusini Dk. Ramphele amezindua chama kipya cha kisiasa kutoa changamoto kwa chama tawala cha ANC kwenye uchaguzi mkuu wa nchi hiyo hapo mwakani.
Dk. Ramphele aliwaambia wafuasi wake waliokusanyika wakati wa uzinduzi wa chama hicho mjini Pretoria kuwa ANC haitakiwi kuaminiwa kuinua uchumi wa nchi hiyo.
Chama chake kijulikanacho kama Agang chenye maana ya kujenga kimejipanga kupigana na rushwa na kuimarisha sekta ya elimu kama malengo  yao makuu.
Dk Ramphele ni mkurugenzi wa zamani wa Benki ya Dunia na ni mke wa zamani wa mpigania uhuru wa Afrika Kusini hayati Steven Biko
 
Habari kutoka gazeti la mwananchi
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...